Diwani wa kata ya Mabira, Mheshimiwa Flarence Rugimbana (CCM), amechaguliwa kwa mara ya pili kushika nafasi ya Makamu Mwenyekiti katika baraza la Madiwani Halmashauri ya Kyerwa.Uchaguzi huo uliokuwa huru na wa haki umefanyika hivi karibuni katika kikao cha Baraza la madiwani ambapo mheshimiwa Rugimbana alipata kura 25 dhidi ya kura 4 za mpinzani wake Mheshimiwa Ndibasa (CHADEMA).
Akizungumza wakati wa kuomba kura kwa wajumbe wa Baraza, Mheshimiwa Rugimbana kupitia chama cha Mapnduzi (CCM) alisema “Waheshimiwa Madiwani, kazi iliyofanyika kwa kipindi cha mwaka mmoja mmeiona, na mafanikio mmeyaona, naombeni nafasi tena nimalizie kazi tuliyoianza”. Naye Mheshimiwa Ndibasa aliyeomba kura kupitia chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) alishukuru Timu ya Menejimenti kwa kuendesha uchaguzi kwa uhuru na Haki na kuwaomba wajumbe kupitia vyama vyote wampe ridhaa ya kuwa Makamu Mwenyekiti, kwani maendeleo hayana chama.
Baada ya uchaguzi wa Makamu Mwenyekiti, ulifuata uchaguzi wa wajumbe wa kamati mbalimbali ambapo Kamati ya Ujenzi, Uchumi na Mazingira, mheshimiwa Joel , Diwani wa Kata ya Nyaruzumbura, alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati. Mheshimiwa Jonas Vedasto Diwani wa Kata ya Kamuli alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Afya, na Mheshimiwa Beneth Byarufu, Diwani wa Kata ya Kimuli alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili.
Aidha, kwa mujibu wa Kanuni , wenyeviti wa kamati wanaingia kamati ya Fedha na Mipango moja kwa moja na pia kanuni inamruhusu Mwenyekiti wa Baraza la Madiwani kuteua wajumbe 4 kuungana na wajumbe wengine kuunda kamati ya Fedha na Mipango baada ya uteuzi huo kuridhiwa na Baraza la Madiwani.Kupitia kanuni hiyo,Mwenyekiti wa Baraza la Madiwani, Mheshimiwa Bahati Henerico ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Rwabwere aliwateua Mheshimiwa Fredrick Bishanga (Diwani kata ya Bugara), Mheshimiwa Aloyce Mwinyi (Diwani kata ya Isingiro),Mheshimiwa Yasinta Katita (Diwani Viti Maalum), na Mheshimiwa Devotha Biashara (Diwani Viti Maalum) kuwa wajumbe wa Kamati ya Fedha.
Kyerwa District Council
Anuani ya Posta: P.O Box 72, KYERWA
Simu ya mezani: +255 686 397 972
Simu ya Mkononi: +255 754 422 746
Barua pepe : ded@kyerwadc.go.tz
Hakimiliki©2017 GWF, Kyerwa District Council. All Rights Reserved